WIZARA ya Fedha na Mipango imesema inatambua na kuthamini mchango mkubwa wa waandishi wa habari katika kuuhabarisha umma kusuhu Sera, Mipango, na Mikakati mbalimbali inayotekelezwa na serikali kupitia wizara hiyo.
Hayo yamesemwa Jijini Arusha na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Benny Mwaipaja, wakati akifungua semina elekezi kwa baadhi ya wahariri wa vyombo vya habari nchini, iliyolenga kuwajengea uelewa wa masuala mbalimbali yanayotekelezwa na Wizara ya Fedha na Mipango.
“Wananchi na umma wa watanzania kwa ujumla hawawezi kupata habari, Wizara inafanya nini, serikali inatekeleza nini bila ya ninyi na wadau wengine wa vyombo vya habari ambao hawako hapa.” Alifafanua Bw. Mwaipaja.
“Kama ambavyo Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, alivyoelekeza Wizara na Idara za Serikali kuwaambia wananchi mambo muhimu ambayo serikali inatekeleza, Sisi kama wizara tuna mambo mengi ya kuwaambia wananchi ikiwemo kuandaa Bajeti Kuu ya Serikali, namna tunavyotafuta rasilimali fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ambayo mmeiona ikiendelea kutekelezwa bila kukwama hii ni kwa sababu ya kazi kubwa inayofanywa na Wizara ya Fedha na Mipango” Alisema Mwaipaja.
Semina hiyo ni moja ya njia za kimkakati katika utekelezaji wa Mkakati wa Wizara wa Mawasiliano (Communication Strategy) ambapo Wizara inakutana na wadau mbalimbali wakiwemo waandishi wa habari. Miongoni mwa mada zitakazowasilishwa ni utekelezaji wa Bajeti ya 2022/2023 na Mwelekeo wa Bajeti Kuu ya Serikali, Utekelezaji wa Sheria ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP),muongozo wa utoaji mafao na pensheni kwa wastaafu na utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs).