Home Afya WAZIRI UMMY; WANANCHI JENGENI UTAMADUNI WA KUPIMA AFYA

WAZIRI UMMY; WANANCHI JENGENI UTAMADUNI WA KUPIMA AFYA

Na Paskal Mbunga, Tanga.

WATANZANIA wametakiwa kujijengea tabia ya kupima afya mara kwa mara badala ya kungoja mpaka waugue kwani, itawasababishia gharama kubwa za kujitibia.

Akizungumza katika ufunguzi rasmi wa kambi ya upimaji afya itakayochukua siku tano jijini Tanga leo, Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu alisema kwamba kumezoeleka tabia kwa watu wengi kutopima afya zao kwa kipindi cha muda mrefu mpaka wapatapo maradhi.

Alisema mazoea hayo ni mabaya kwani yamewasababishia watu wengi kuingia gharama za matibabu wanapougua ambapo wakati mwingine hushindwa kulipa na hivyo kuwaingiza katika matatizo ya kutopata matibabu yanayostahili.

Ummy Mwalimu ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Tanga Mjini, alibainisha kuwa ulaji wa aina ya vyakula unaweza ukawa ni sababu ya kupata maradhi.

“Tumezoea kula vyakula vyenye mafuta mengi tukiamini hicho ndicho chakula bora kumbe tunajichimbia wenyewe kaburi la kifo kutokana na kuzidisha mafuta ambayo ndiyo kisababishi cha madhara ya afya yetu”, alitahadharisha.

Waziri alitaja baadhi ya vyakula vinavyotumiwa na watu kwa wingi tena kwa mazoea kuwa ni pamoja na sukari au chumvi iliyopitiliza.

Aliwataka Watanzania kufanya mazoezi ya miili ikiwa pamoja na kutembea, kukimbia au hata kuzunguka nyumba unayoishi mara kadhaa ili mradi utokwe jasho.

Aliwahakikishia wakazi wa Tanga kuwa ataendelea kuwatumikia kwa moyo mkunjufu ikiwa ni pamoja na kushirikiana na taasisi/mashirika ya ndani na nje ili kuleta huduma mbalimbali zihusuzo afya na matibabu.

Mratibu wa Taasisi ya AfyaCheck, Dr. Isack Maro alisema katika siku tano watakazoendesha zoezi hilo, mkazo mkubwa utawekwa katika magonjwa yasiyoambukiza ambayo ni pamoja na magonjwa ya Pressure na Kisukari.

Alisema amevutiwa sana na mwitikio wa watu katika zoezi hilo kwani makisio ya awali ilikuwa angalau watu 400 wangehusika, lakini kwa leo (jana) pekee waliojiorodhesha wamefikia watu 1400.

“Kwa hali hiyo inaonesha huenda idadi ya watu watakaohudumiwa wakafikia zaidi ya 5,000″

Mwisho

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here
Captcha verification failed!
CAPTCHA user score failed. Please contact us!