Home Kitaifa TANZANIA NA SAUDI ARABIA KUSHIRIKIANA KATIKA SEKTA YA MAFUTA NA GESI

TANZANIA NA SAUDI ARABIA KUSHIRIKIANA KATIKA SEKTA YA MAFUTA NA GESI

📌Serikali kuimarisha maghala ya mafuta nchini

📌Dkt. Biteko akaribisha uwekezaji wa uzalishaji wa dawa za mifugo

Na Ofisi ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amesema kuwa Serikali ina nia ya kuimarisha miundombinu ya maghala ya kuhifadhia mafuta kwenye bandari za Tanga na Mtwara.

Alisema hayo jana Juni 19, 2024 jijini Dodoma wakati akizungumza na Mbunge wa Bunge la Maldives, Mhe. Ibrahim Muhammad.

“Kwa miaka miwili sasa Tanzania inashirikiana na Saudi Arabia kupitia Kampuni yake ya ARAMCO, huu ni ushahidi wa uhusiano wetu imara. Kwa sasa maghala yetu makubwa yapo Dar es Salaam hata hivyo tuna nia ya kupanua miundombinu ya maghala yetu ya kuhifadhi mafuta katika bandari ya Tanga na Mtwara. Upanuzi huu utaimarisha uwezo wetu wa usambazaji wa mafuta nchini,” amesema Dkt. Biteko.

Aidha, kuhusu gesi Dkt. Biteko ametaja baadhi ya fursa hasa katika gesi iliyochakatwa (CNG) na kuwa Serikali imeendelea kukuza matumizi ya nishati safi ya kupikia.

“Tanzania imeanza Kampeni ya Nishati Safi ya Kupikia ikilenga kuondoka kwenye matumizi ya magari yanayotumia mafuta na kutumia magari yatakayotumia nishati ya gesi asilia. Kwa sasa ni asilimia 6 tu ya wananchi ndiyo wanatumia gesi ya kupikia, hivyo Serikali ina mpango wa kukuza matumizi ya gesi asilia nchini na Tanzania inatarajia kufanya kazi kwa karibu na Saudi Arabia pamoja na Maldives ili kuendelea kutumia fursa hizi kikamilifu.” Amesema Dkt. Biteko.

Akizungumzia uwekezaji katika kiwanda cha kuzalisha dawa za kuku, Dkt. Biteko amewakaribisha wawekezaji wa dawa hizo kutoka nchini Misri na kusema kuwa Tanzania na Misri ni washirika wa muda mrefu na nchi hizo zina uhusiano wa kihistoria na kuwa Tanzania ni nchi nzuri ya kuwekeza kwa kuwa ina soko la uhakika.

Katika hatua nyingine, Mbunge wa Bunge la Maldives, Mhe. Ibrahim Muhammad ameeleza nia yake ya kuwekeza katika sekta ya nishati nchini Tanzania kupitia nchi ya Saudi Arabia na kusema kuwa uwekezaji huo utaimarisha uhusiano wa nchi hizo tatu.

Aidha, kikao hicho kimehudhuriwa na Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Musa Zungu na ujumbe kutoka nchini Misri.

Mwisho.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here
Captcha verification failed!
CAPTCHA user score failed. Please contact us!