- OPARESHENI KALI KUENDELEA
Na Shomari Binda-Tarime
MKUU wa Mkoa wa Mara Said Mtanda ametoa tahadhari kwa wananchi watakaoendeleza kilimo cha zao haramu la bangi wilayani Tarime.
Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika Kata ya Nyamongo wilayani humo amesema kamwe kilimo cha bangi hakiwezi kukubalika mkoani Mara.
Amesema hadi sasa kwa oparesheni ambazo zimefanyika mkoani Mara zaidi ya ekali 200 zimeteketezwa na watu kadhaa kukamatwa.
Mtanda amesema kwa mujibu wa sheria ya sasa ya madawa ya kulevya adhabu yake ni pamoja na kifungo cha miaka 30 jela au maisha.
Amesema kwa wale watakaokaidi na kuendelea na kilimo hicho wataziacha familia zao na kwenda kutumikia vifungo.
“Nimekuja kuwakumbusha mambo kadhaa ikiwa ni pamoja na kutoa tahadhali juu ya kilimo cha zao haramu la bangi hapa Tarime”
“Sheria za sasa ni kali hivyo tusiendelee kushiriki kwenye kilimo hiki kwa kuwa tutaziacha familia zetu na kwenda kutumikia vifungo jela na hivi karibuni oparesheni kali itaendelea” amesema.Mtanda.
Akizungumzia hali ya usalama amesema kwa sasa ni shwali na hakuna matukio yoyote ya uvunjifu wa amani yaliyo lipotiwa.
Amesema mwananchi ndio mlinzi wa kwanza wa amani na kuwataka kushirikiana na viongozi wa ngazi mbalimbali ili kuimalisha usalama kwenye maeneo yao.
Aidha mkuu huyo wa mkoa amesisitiza wazazi na walezi kuhakikisha kila mtoto anayestahili kwenda shuleni anakwenda hata kama hana sare za shule wakati zikiendelea kutafutwa