Home Kitaifa NAIBU WAZIRI SILINDE ASHUHUDIA UJIO WA NEEMA KUBWA SEKTA YA KILIMO...

NAIBU WAZIRI SILINDE ASHUHUDIA UJIO WA NEEMA KUBWA SEKTA YA KILIMO , MKATABA KATI YA EQUITY BENKI , PASS NA MCODE

Naibu Waziri wa Kilimo Mhe. David Silinde ( aliyesimama kati kati ) akishuhudia utiaji saini mkataba wa mashirikiano (MOU) kati ya taasisi tatu ambazo ni EQUITY Benki , Taasisi ya Biashara ya PASS na Taasisi ya MCODE zenye lengo la kuboresha maisha ya watanzania hasa  wakulima. Mkataba huo umesainiwa katika Viwanja vya Maonesho ya Nane Nane Jijini Dodoma , wanaosaini ( waliokaa ) ni Meneja Mkuu wa Biashara wa Benki ya Equity Bi. Leah Ayoub na Mkurugenzi wa Biashara kutoka Taasisi ya PASS Bw. Adam Kamanda.

Na Mwandishi Wetu.

WAKULIMA nchini wameshauriwa kuchangamkia fursa mbalimbali zinazotolewa na taasisi za kilimo pamoja na kibenki zinazolenga kuwawezesha kukuza mnyororo wa thamani katika sekta na hatimae kuchangia pato la taifa.

Haya yameelezwa Mkoani Dodoma katika maonesho ya Kilimo, Uvuvi na Ufugaji maarufu Nane Nane na wadau wa fedha na kilimo wakati Naibu Waziri wa Kilimo Mhe. David Silinde akishuhudia utiaji saini mkataba wa mashirikiano MOU  kati ya taasisi tatu ambozi ni EQUITY Benki ,taasisi ya biashara ya PASS na taasisi ya MCODE zenye lengo la kuboresha maisha ya watanzania hasa  wakulima.

Akizungumza mara baada ya utiaji saini makubaliano hayo, Meneja Mkuu wa Biashara wa benki ya Equity Bi. Leah Ayoub amesema mkataba huo una lengo la kuboresha maisha ya watanzania hasa wakulima walioko vijijini wanaohitaji kupata huduma za kifedha hususani mikopo lakini hawana dhamana za kupata mikopo ,hivyo makubaliano haya yatawawezesha kupata dhamana za mikopo pasipo gharama yeyote.

Naye mkurugenzi wa biashara kutoka taasisi ya PASS Bw. Adam Kamanda ameeleza  kuwa mikataba hiyo ni kwa ajili ya uendelevu kibiashara ambapo watawasaidia wakulima kulima kisasa , ili kuongeza tija katika mazao yao na kukuza mnyororo wa thamani kwenye sekta ya kilimo, ambapo mpaka sasa wamefikiwa wakulima  elfu 30 na lengo ni kufikia watu zaidi ya laki moja.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi inayotekeleza mradi wa kuwawezesha wakulima wadogo kupata usaidizi wa kifedha MCODE Ndg. Slaiton Kaberege amesema kuwa pamoja na hayo pia wanawezesha wakulima kupata   pembejeo, na mpaka sasa wamekwisha Pata mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 20 wakiwa na vikundi elfu moja kwenye mikoa sita.

Benki ya Equity inaamini kupitia uwezeshaji wa wakulima wadogo wadogo walio katika vikundi kutaiwezesha benki kufikisha huduma za kifedha kwa wananchi wengi zaidi hivyo kutimiza adhima ya serikali ya kuboresha sekta ya kilimo ambayo imeajiri watu wengi na yenye mchango mkubwa zaidi katika pato la taifa. 

Ni dhamira ya Benki ya Equity kufanya kazi na wadau wote wenye malengo na maono yanayoendana na Serikali katika kuhakikisha inachangia juhudi za serikali kwenye sekta ya kilimo hasa hasa Agenda 2030.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here
Captcha verification failed!
CAPTCHA user score failed. Please contact us!