Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Dkt. Rashid Mfaume ameitaka Hospitali ya Taifa Muhimbili Mloganzila kuendelea kuwajengea uwezo wataalamu wa Hospitali za Rufaa za Mikoa (RRH) ili kuweza kusaidia upatikanaji wa huduma za kibingwa kwa wananchi.
Dkt. Mfaume amesema hayo wakati wa ufunguzi wa kambi ya uchunguzi na matibabu inayoendeshwa na Madaktari Bingwa wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Mloganzila kwa kushirikiana na Madaktari wa Hospitali ya Mwananyamala inayoendelea katika viwanja vya Hospitali ya Mwananyamala mkoani Dar es Salaam.
“Wananchi wa Wilaya ya Kinondoni na maeneo jirani changamkieni fursa ya kupata huduma, kambi hii ni ya kipekee tofauti na zile ambazo huwa zinafanyika viwanjani, wataalamu wamekusanyika hapa kuna maabara, vipimo vya ECG na ECHO na Radiolojia, mgonjwa anapokelewa anafanyiwa vipimo, tatizo lake likibainika anapewa matibabu hapa tena kwa gharama nafuu, kama anahitaji rufaa anapelekwa Mloganzila, ” amesema Dkt. Mfaume
Amesema Hospitali za RRH zina wataalamu bingwa lakini wataalamu bobezi ni wachache, hivyo ni fursa pia kwa wataalamu wa Mwananyamala kujifunza.
Akizungumza Kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji Hospitali ya Taifa, Naibu Mkurugenzi Mtendaji Muhimbili Mloganzila Dkt. Julieth Magandi amesema kuwa moja ya jukumu la Hospitali ya Taifa ni kuwajengea uwezo wataalamu wa Hospitali za ngazi za chini katika maeneo mbalimbali hivyo anaamini kupitia kambi kama hizi zitatimiza lengo hilo ambalo pia ni agizo la Wizara ya Afya.
“Huu ni mwanzo tu, tutafanya kambi hizi katika Hospitali Rufaa za Mikoa ambazo ni Temeke na Tumbi na baadaye tunahamia kwenye mikoa mingine pia suala la kufanya kambi za matibabu litawekwa kwenye mpango kazi wa mwaka wa Hospitali ya Mloganzila ili lifanyike Kwa ufanisi zaidi” amesema Dkt. Magandi
Kwa upande wake Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mwananyamala Dkt. Aileen Malongo amesema kuwa muitikio wa wananchi katika kambi ni mkubwa na kwamba huduma zinatolewa na Madaktari bingwa bobezi katika kada sita ambazo ni macho, magonjwa ya damu, moyo, kisukari, mfumo wa mkojo pamoja na mifupa.
“Kambi hii itafanyika kwa siku nne ambapo imeanza tarehe 9, na itandelea 10, 11 na 13 Januari 2023, gharama zimepunguzwa sana ili wananchi waweze kunufaika” amesema Dkt. Aileen
Kwa upande wake Mwl. Mansoor Nkondo ambaye amefika kupata huduma katika kambi amesema kuwa amepata matibabu kwa gharama sawa na bure.