NA IS-HAKA OMAR,ZANZIBAR.
MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambaye pia ni Rais Wazanzibar Dk Hussein Mwinyi amesema ipo haja ya watendaji kuzingatia ndani ya chama kuzingatia vijana wa UVCCM wanaojitolea zinapotokea fursa za ajira.
Dk Mwinyi ametoa kauli hiyo jana Gymkana wakati akihitimisha ziara yake ya kutembelea mali za chama hicho na Jumuiya zake katika Mkoa wa Mjini ambapo alisema anajua kilio cha vijana wengi kukosa ajira.
“Ntambua ninyi ni wapiganaji mnajitolea kwahiyo napenda kuwahidi kwamba kuna mipango mingi ya kutengeza ajira na mtapata hasa nyie mliojitoea kwa muda mrefu,” alisema
Dk Mwinyi alisema anayo mipango ya kuzalisha ajira nyingi na kuwachukua vijana wengi hivyo wasivunjike moyo.
Dk Mwinyi alisema vijana hao wamefanya kubwa lakini kuna wakati wamekata tamaa huku akiwasihi waendelee na moyo huyo.
Kuhusu miradi ya CCM alisema ni lazima waangalie vyema mali hizo na wawe na miradi mikubwa ya kukiendesha chama kiuchumi.
Alisema jumuiya zote za chama hicho lazima ziwe na ofisi za kisasa na majengo yanayoendana na hadhi ya chama hicho katika ngazi zote.
Kwa mujibu wa Dk Mwinyi, baada ya ziara amepata mtazamo mzuri kuhusu rasimali za chama hicho hivyo watafanya mambo makubwa ya kukifanya chama kiwe na uwezo mkubwa kama vyama vingine duniani.
Alisema chama kina chnagamoto nyingi ikiwa ni pamoja na ukosefu wa vifaa, miundombinu na vyombo vya usafiri.
Awali Naibu Katibu Mkuu wa UVCCM Zanzibar, Musa Haji Mussa alisema jumuiya hiyo wanamipango na ndoto kubwa za kufanya uwekezaji wa miradi mbalimbali lakini bado haijafikiwa na imani yao ndoto hizo zitafikiwa kupitia kwake (Mwinyi).
Katibu wa CCM Mkoa wa Mjini Suleiman Tate alisema wanapata hofu ya eneo la mradi katika ofisi hiyo ya Mkoa huo huenda likapitiwa na mradi wa kujenga barabara za juu unaotarajiwa kujengwa hapo Amani hivyo kupoteza moja ya vitega uchumi.
Katika ziara hiyo Dk Mwinyi alitembelea maduka an sehemu ya vileo Amani, eneo la maduka youth League darajani, sheli na eneo la umoja wa vijana Gymkana.