Na Shomari Binda-Musoma
MWENYEKITI wa Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Mara Patrick Chandi amezindua kampeni za udiwani Kata ya Mshikamano manispaa ya Musoma.
Akizindua kampeni hizo mtaa wa Saa nane amesema CCM inayo hazina ya viongozi wazuri wakiwemo vijana na mgombea waliyemsimamisha wamempima na anao uwezo wa kuongoza.
Amesema Kata ya Mshikamano wamepata kijana anayeweza kutumwa akakimbia na kuwaletea wananchi maendeleo.
Chandi amesema wananchi wa Mshikamano wamuamini na kumchagua Njofu Constantine Katama kwani ni kijana aliyepikwa kiuongozi na ni mwadilifu.
“Chama cha Mapinduzi hakiwezi kuwaletea kiongozi wa hovyo huyu ni kijana safi mwenye maadili na rekodi zake za uongozi zipo vizuri”
“Naomba siku ya terehe 20 mwezi huu twende tukamchague Njofu ili ashirikiane na madiwani wengine wa CCM atuletee maendeleo” amesema.
Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Musoma mjini Benedict Magiri amesema wananchi wa Kata ya Mshikamano wanayo bahati ya kuletewa mgombea ambaye anaijua Kata hiyo.
Amesema Njofu Constantine atakwenda kushirikiana na madiwani wengine wa CCM kuhakikisha wananchi wanafikiwa na maendeleo kusudiwa.
Mgombea wa udiwani Kata hiyo ya Mshikamano kupitia CCM Njofu Constantine amewaomba wananchi wamuamini kama alivyoaminiwa na chama chake kwa kuwa anao uwezo wa kuongoza.
Amesema kwa kuwa ni mzaliwa wa Mshikamano anazijua changamoto na atakwenda kwenye baraza la madiwani na kuzieleza ili ziweze kupatiwa ufumbuzi.