Home Kitaifa RAMLI CHONGANISHI IKOMESHWE

RAMLI CHONGANISHI IKOMESHWE

Na Neema Kandoro Mwanza

ZAIDI ya waganga wa tiba asili 450 Mkoani Mwanza wametaka kuwepo na njia madhubuti kuzuia waganga wanao piga ramli chonganishi ambazo zinatajwa kuchochea uhasama na kusababisha mauaji kwenye jamii.

Waliyasema hayo katika kikao kilichokutanisha waganga, watemi na Jeshi la polisi toka halmashauri zote mkoani hapa jijini Mwanza, kutathimini mwenendo wa suala la usalama kutokana na waganga hao kuenenda kwa mjibu wa sheria za nchi ambapo umepunguza vitendo vya uhalifu.

Kamanda wa Jeshi la polisi Wilbroad Mtafungwa alisema kundi hilo ni mhimu katika kuimarisha misingi ya amani na utulivu ambapo alikemea baadhi ya waganga kufuatwa na wahalifu ili wapatiwe dawa za kuficha uhalifu waliofanya.

Nawahakikisheni kuwa ushirikiano wenu na sisi ni muhimu katika kujenga mkoa wetu kwa utulivu na amani” alisema Mtafungwa.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Umoja wa Watemi wa Usukuma Charles Balele maarufu kama Ntemi Itale alilipongeza jeshi la polisi kuwaita na kujadiliana namna ya kuenenda kazi zao kwa utaratibu.

Alisema dosari na changamoto zilizojadiliwa zitasaidia kuondoa ama kumaliza tatizo la uwepo wa waganga wanaopiga ramli chonganishi kupitia udhibiti wa leseni zinazotolewa kwa waganga.

Mganga wa tiba asili Nyashana Jijini Mwanza, Msaku Chibuga aliomba Mamlaka zinazohusika kutokamata vitendea kazi vyao ambavyo wanatumia katika kazi kwa kisingizio cha kuwa nyara za serikali bali uangaliwe utaratibu wa kutumia.

Alisema baadhi ya vitu hivyo wamerithishwa na wazee wao muda mrefu hivyo kitendo cha wao kukamatwa kinawavunja moyo katika kufanya shughuli zao kwani nyara vilevile huuzwa na mamlaka husika.

Mwenyekiti wa Waganga wa Tiba Asili Kanda ya Ziwa Jesca Mwendesha aliomba watemi wahusishwe katika utoaji wa vibali kwani wanawafahamu waganga wa kweli kwa kuwa ni viongozi wao wa jadi.

Alisema waganga ambao hawafanyi kazi zao kwa kuzingatia sheria na utaratibu wanaharibu fani yao ya kutumikia watu kwa uadilifu kama inavyotegemewa na jamii ya watanzania.

Mganga wa Tiba Asili Nyakato Jijini Mwanza, Braiton Mwiga amewataka waganga kupata leseni ili kuepuka kufanya shughuli zao kinyume cha sheria.

Aidha amewasisitiza waganga wote kushirikiana na serikali ili kujenga amani na utulivu katika maeneo yao.

Mwenyekiti Msaidizi Shirikisho la Vyama vya Waganga Tanzania (SHIVYATIATA) Ayoub Omoro alishauri usajili wa waganga uchukue muda mfupi na kuondolewe utaratibu wa kulipia kwenye vyama vyao kupata leseni kitu ambacho ni adha katika shughuli zao.

Katibu wa watemi Tanzania Aroun Mikomangwa amwewahasa waganga kuongeza elimu ili waweze kuhudumia vizuri wagonjwa na kujikinga dhidi ya maradhi wanapohudumia.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here
Captcha verification failed!
CAPTCHA user score failed. Please contact us!