Na Shomari Binda-Musoma
WENYEVITI wa mitaa nchini wameshauriwa kutumia mikutano yao kutoa elimu ya ufahamu juu ya Katiba ya nchi.
Ushauri huo umetolewa na kada wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na mjumbe wa zamani wa Mkutano Mkuu wa UVCCM Ibrahimu Omari alipozungumza na Mzawa Blog.
Amesema wananchi wanapaswa kuwa na uelewa wa masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na uzungumzaji kwa kuzingatia sheria na taratibu.
Kada huyo amesema Katiba ya nchi ibara ya 146 (2b) inazungumzia masuala ya serikali za mitaa na majukumu yake kwa wananchi.
Amesema kwenye ajenda zao kwenye mikutano wanapaswakuwa na ajenda ya kutoa elimu juu ya uelewa wa Katiba, Sheria, Kanuni na taratibu mbalimbali za nchi.
“Wenyeviti wa mitaa ndio wanaoishi na wananchi kila siku na wanakutana kwenye mikutano ya hadhara hivyo ni muhimu kuwapa elimu”
“Wananchi wamekuwa wakitoa maoni yao kwenye masuala mbalimbali lakini wengi wao wamekuwa hawatoi maoni kwa kuzingatia taratibu“, amesema Ibrahim
Amesema taifa kwa sasa lina mjadala wa bandari bila kuwa na uelewa wananchi watabaki njia panda kwenye uchangiaji.