Home Kitaifa TUYAENZI MEMA YA MAREHEMU BERNARD MEMBE-RAIS DKT SAMIA

TUYAENZI MEMA YA MAREHEMU BERNARD MEMBE-RAIS DKT SAMIA

*Asema atakumbukwa na Jumuiya za Kimataifa kwa utumishi wake

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amewaomba watanzania kumuombea na kuenzi yote mazuri aliyowahi kufanya marehemu Bernard Kamilius Membe enzi za uhai wake.

Amesema hayo leo Jumanne (Mei 16, 2023) alipomuwakilisha Rais Dkt. Samia katika ibada ya mazishi ya Marehemu Bernard Membe iliyofanyika kijijini kwake Chiponda, Rondo Mkoani Lindi

Watanzania, Wanalindi na hapa Rondo, Mheshimiwa Rais Samia amewataka muenzi yale yote mema aliyotenda wakati wa uhai wake, lakini pia endeleeni kumuombea ili mwenyezi Mungu amlaze mahali pema

Waziri Mkuu amesema kuwa Rais Dkt Samia amesema kifo cha Bernard Membe kimewaacha watanzania na Wana-Lindi na butwaa kubwa, simanzi na huzuni, “Amesema anatoa pole sana kwa wote walioguswa na msiba huu ndani na nje ya nchi yetu”

Rais Samia amesema kuwa Marehemu Membe atakumbukwa kwa mengi na watanzania na jumuiya za kimataifa kutokana na utumishi wake uliotukuka katika nafasi mbalimbali alizohudumu wakati wa uhai wake

Marehemu Membe atakumbukwa kwa usikivu wake, upole na weledi katika kufanya majukumu yake, uzalendo wa Taifa na mwenye msimamo thabiti, alikuwa mfano mzuri wa kuigwa

Aidha, Mheshimiwa Majaliwa amewataka wana-Rondo kumuezi Membe kwa kutunza yale yote aliyoyaanzisha na kuyasimamia katika eneo hilo.

Kwa upande wake Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne Dkt. Jakaya Kikwete amesema kuwa Marehemu Bernard alikuwa Mwanadiplomasia mbobezi, Mwanamikakati makini na mchumi mzuri

Amesema kuwa katika kipindi cha Miaka tisa akiwa Waziri wa Mambo ya Nje alifanya kazi kubwa ya kuendeleza maslahi ya Tanzania katika medani za Kimataifa na kikanda”

Naye Mbunge wa Jimbo la Mtama na Waziri wa Habari,Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mheshimiwa Nape Nnauye amesema kuwa Membe alikuwa mwalimu wa wengi, mzalendo, jasiri na mwenye mapenzi makubwa kwa nchi “Sisi wanafunzi wake tutalinda, tutadumisha na kuendeleza kila aliloliweka na kuliwekeza kwetu”

Marehemu Bernard Membe ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa alifariki Mei 12, 2023 katika hospitali ya Kairuki Jijini Dar es Salaam

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here
Captcha verification failed!
CAPTCHA user score failed. Please contact us!